
Tanzia kwa Mwana wa Afrika
Tujifunze kutoka kwa Kanyama Chiume
NI wiki moja kamili sasa tangu Afrika impoteze mmoja wa majemedari wake wa mwisho na mwasisi wa mapambano ya uhuru na umoja wa kweli wa Afrika, Mzee Kanyama Chiume akijulikana kabla ya hapo kama, Murray William Kanyama Chiume (78).
Mzee Chiume alifariki dunia Jumatano iliyopita akiwa New York Marekani, ambako alikuwa akiishi kwa miaka kadhaa na baadhi ya watoto wake walio huko kikazi.
Kwa hakika kifo cha shujaa huyu wa Malawi, Tanzania na Afrika nzima kinalifanya bara hili kuendelea kupoteza baba mmoja baada ya mwingine wa vita vya ukombozi na waasisi wa mapambano ya umoja wa Afrika.
Kabla ya kifo chake cha wiki iliyopita, Afrika ilikuwa imebakiwa na yeye na Rais wa zamani wa Zambia, Kenneth Kaunda.
Bila ya kutafuna maneno, viatu vya Chiume vilikuwa vikiwatosha wanasiasa wa kariba yake; akina Kwame Nkrumah, Julius Nyerere, Jomo Kenyatta, Sekou Toure na wachache wengine ambao idadi yao haizidi wanafunzi 12 wa Yesu Kristo.
Wakati Baba wa Taifa alipokuwa ndiye kiongozi wa harakati za mapambano ya uhuru wa Tanganyika miaka ya mwanzoni mwa 1950, Chiume ndiye aliyekuwa kinara nchini Malawi, akiwa ndiye mwakilishi wa chama cha Nyasaland Congress Party kilichokuja kujulikana baadaye kama Malawi Congress Party.
Kupitia katika chama chake hiki, yeye ndiye aliyekiwakilisha katika mikutano ya kimataifa kule London, Accra Ghana na Tanzania.
Alishiriki kikamilifu katika uanzishwaji wa vuguvugu la kudai uhuru kwa pamoja kwa mataifa ya Kiafrika akiwa mjumbe wa Malawi katika mkutano uliozaa lile la nchi zilizo Afrika ya Mashariki na Kati (Pafmeca) kule Mwanza na baadaye Pafmecsa ukijumuisha na nchi za kusini.
Alikuwa miongoni mwa viongozi wa Kiafrika waliokutana mara kadhaa kwa ajili ya kuanzisha uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU) na mwaka 1964 katika mkutano uliofanyika Cairo Misri, hotuba kali ya kimapinduzi ndiyo iliyomkera rais wake Kamuzu Banda na kumjenga uhasama.
Nilipokutana naye kwa mara ya kwanza, Mzee Chiume alipata kunisimulia kuhusu mzozo mkali wa maneno uliozuka kati ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Rais wa Kwanza wa Ghana, Kwame Nkrumah ambao ulitishia uhai wa OAU.
Leo hii miaka takriban 10 tangu anieleze kuhusu tukio hilo alilolielezea kuwa ni baya kuliko yote katika uhai wa OAU, bado naweza nikakumbuka kwa ufasaha maneno aliyonieleza.
“Bado naikumbuka siku hiyo vyema kabisa. Ilikuwa ni siku ngumu kwetu. Viongozi wetu wawili, tuliokuwa tukiwaheshimu na kuwasikiliza, walizozana kweli kweli. Mwalimu alikuwa akipinga mtazamo. Sijapata kumuona Mwalimu akiwa amekasirika kama siku hiyo. Ugomvi ule ungeweza kuimega OAU,” alinieleza Chiume aliyekuwa akizungumza Kiswahili kwa ufasaha kabisa huku akivuta tukio moja baada ya jingine.
Katika mazungumzo yake siku zote, Chiume alikuwa akiiona Afrika kuwa moja na mipaka ya kikoloni haikuwa kikwazo cha kuwafanya Waafrika kupigana.
Ninapokumbuka maneno mengi mazito niliyoyasikia kutoka kwa Chiume miaka 1o iliyopita na kupekua pekuwa makabrasha ya historia ya bara hili, kwa mfano wa maneno ya Yohana Mbatizaji, napata shida kuwafunga kidamu za mzee huyo viongozi wa zama hizi wa Bara la Afrika.
Watoto wadogo na Watanzania wasioijua vyema historia ya mapambano ya uhuru wa Malawi na ile ya Afrika ya kati ya miaka ya 1950 hadi 1960 wanaweza wakashangaa, jina la mwanasiasa huyu likitajwa na kuwekwa katika mizania ya wanasiasa wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere.
Chiume na wenzake wengine kadhaa akiwamo rafiki yake mkubwa Henry Chipembere na Orton Chirwa wanaweza wakatajwa kuwa ndiyo viongozi waasisi wa mapambano ya uhuru wa Malawi.
Chiume ambaye miaka ya mwanzoni mwa 1950 alikuwa na umri usiodizi miaka 25 na wenzake zama hizo wakijulikana kwa jina kwa jina la Kiingereza ‘The Young Turks’ (Vijana wasiodhibitika).
Nilipokutana naye katika kipindi cha kati ya mwaka 1996 wakati huo akija hapa nchini mara kadhaa baada ya kurejea Malawi miaka miwili iliyotangulia, nilipata fursa ya kujifunza mambo mengi kuhusu maisha ya mwanasiasa huyu na namna alivyoshirikiana na wenzake wengine katika vita ya mapambano ya ukombozi wa Afrika.
Mzee Chiume alinipa fursa ya kuijua historia ya Malawi, Tanzania na Afrika, nje ya ile tunayosoma katika vitabu na maandiko mabalimbali ya kihistoria.
Ndani ya akili yake, mzee huyo ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 66, alikuwa na kumbukumbu sahihi ya matukio mbalimbali yaliyokuwa yakitokea zama za harakati za kudai uhuru wa nchi yake na ule wa Afrika.
Kwa hakika nikiwa mwanafunzi wa historia zama hizo, mzee huyu aliongeza ufahamu wangu kuhusu historia iliyopotoshwa ya harakati za ukombozi wa bara la Afrika.
Kupitia kwake nilimfahamu Kamuzu Banda, Rais wa kwanza wa Malawi ambaye miaka 30 ya utawala wake wa kiimla, aliiondoa nchi yake kuwa miongoni mwa mataifa ya mwanzo kabisa kudai na kupigania uhuru si wa taifa moja moja la Afrika bali la Afrika.
Kwa maneno yake mwenyewe Mzee Chiume aliniambia kuwa alikuwa akijutia uamuzi wake yeye na mwenzake Chipembere wa kusikia ushauri wa aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Ghana, Kwame Nkrumah wa kuwataka wao wamkubali Banda kuwa kiongozi wa harakati zao za ukombozi wa Malawi.
Wakiwa wadogo kiumri, Chiume na Chipembere waliheshimu maoni hayo ya Nkrumah wakihadaika na ushiriki wa Banda katika harakati za mwanzoni kabisa za mshikamano wa Waafrika (Pan African Movement).
Kama ilivyokuwa kwa Nkrumah na kwa vijana hao ambao walikuwa wameshaasisi mapambano ya uhuru wa nchi yao, Banda wa zama hizo, miaka ya 1940 na 1950 alibeba taswira ya kweli ya mwana wa Afrika, mpigania uhuru mwenye uchungu na nchi yake na bara lake.
Ni jambo la bahati mbaya kwamba, uamuzi wa Banda kuhudhuria mkutano wa kwanza wa Mwamko wa Afrika (PanAfrican Congress) mwaka 1945 kule Manchester, Uingereza akiwa na Kenyatta na Nkrumah ulimfanya aonekane kuwa mmoja wa wanamapinduzi hodari na wa kuaminika wa Kiafrika. Ukweli haukuwa huo.
Mzee Chiume alinieleza namna Banda alivyoweza kutoka ndani ya gamba alilojificha kwa zaidi ya miaka 10, kwnai miezi isiyozidi mitatu tangu Malawi ipate uhuru wake mwaka 1964, ghafla alibadilika na akawa mpinzani mkubwa wa misingi ya ukombozi wa taifa lake na ule wa bara lake.
Akina Chiume walipigwa na butwaa kumuona Banda akitangaza kuutambua utawala wa kibaguzi wa makaburu wa Afrika Kusini ambao ulikuwa umetengwa na jumuiya ya kimataifa na miaka michache baadaye akaingia katika mzozo na Tanzania akigombea sehemu ya ardhi yetu.
Chiume, wakati huo akiwa Waziri wa Mambo ya Nje akiungwa mkono na mawaziri wenzake wengine watano, walikataa kumtii Banda, na matokeo yake wakafukuzwa kutoka serikalini.
Hali hii haikuishia hapo, Banda ambaye alishawatangaza kuwa ni wasaliti, akafanya jaribio la kuwakamata na kuwaua, tukio ambalo liliwanasa watu kadhaa na kumkosa Chiume ambaye kwa msaada wa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere alifanikiwa kutorokea Tanzania.
Kama ilivyokuwa kwa wana mapinduzi wengine kadhaa wa Kiafrika Chiume akarejea Tanzania ambako alisomea na kukulia na akaishi katika kipindi chake chote cha miaka 30 akiwa mkimbizi.
Nilipozungumza naye kuhusu matukio hayo, Chiume alikiri kufanya kosa kubwa la kumruhusu Banda kuziteka nyara harakati zao za mapambano ya uhuru wa Malawi nay ale ya Afrika.
Kwa hakika, kama si hulka yake ya kutopenda madaraka na kuwa tayari kusikiliza ushauri wa wanamapinduzi wenzake, Chiume alikuwa na nafasi kubwa ya kuwa Rais wa kwanza wa Malawi huru na mmoja wa viongozi ambao kifo chake kingewekwa katika daraja moja na akina Nyerere na Nkrumah hata na wale ambao hawakupata kumfahamu.
Wakati nikizungumza naye miaka 10 iliyopita, kulikuwa na maneno ya chinichini yalikuwa yakidai kuwa, Banda halisi aliyechukuliwa na Waingereza na kupelekwa Afrika Kusini na baadaye Uingereza hakuwa yule yule aliyerudi Malawi na kuwa Rais wa Kwanza wa Taifa hilo dogo lililo Kusini Mashariki mwa Afrika.
Nilipozungumza naye kuhusu tetesi hizo, Mzee Chiume alinihakikishia kuwa alikuwa ameshaanza kulifanyia uchunguzi suala hilo na kimsingi alitaka kuandika kitabu juu ya kile kilichotokea Malawi na hadaa ya Banda iliyomwezesha kuupata urais wa Malawi. Sikupata kujua iwapo alitimiza lengo lake hilo.
Amefariki akiwa na mapenzi makubwa kwa taifa lake na kwa Bara lake na ndiyo maana aliporejea nchini mwaka 1994, alianzisha chama cha upinzani akikiita Congress for Second Republic (CSR), akiamini kuwa taifa hili lilikuwa likihitaji uhuru wa kweli.
Tangu wakati huo akawa mstari wa mbele kupigania uimara ya mfumo wa vyama vingi na akatumia muda wake mwingi kuwaasa Wamalawi wenzake kutokubali tena kuirejesha nchi yake katika udikteta wa chama kimoja. Utawala wa mkono wa chumba wa Banda ukampa fundisho kubwa.
Tanzania
Chiume hawezi kutenganishwa na Tanzania. Historia yake ya maisha yake binafsi, kifamilia na kisiasa yanaungana moja kwa moja na taifa hili.
Mwandishi mwenzangu Maggid Mjengwa katika blogu yake ameonyesha kwa ufasaha namna Mzee huyu alivyo na uhusiano na taifa hili. Maggid anaanza kwa kusema;
Huyu mzee alisoma katika shule mbalimbali hapa nchini kuanzia elimu yake ya msingi hadi ile ya Sekondari kabla ya kwenda Chuo Kikuu cha Makerere alikosomea ualimu.
Aidha hata alipokuja kuishi ukimbizini, alioa mke wa Kitanzania akazaa watoto wake akina Nathan na ndugu zake wengine Tanzania. Wamesoma Tanzania na kimsingi wana Utanzania.
Akiwa ukimbizi hapa nchini, Chiume alikuwa akifanya kazi ya uandishia na makala zake za kimapinduzi zilikuwa zikichapwa katika magazeti mbalimbali kuanzia The Nationalist (baadaye Uhuru na Mzalendo) na katika gazeti la serikali la Daily News.
Si hayo tu, hata kabla ya uhuru wa Malawi, Chiume akiwa mjumbe wa Vuguvugu la Kudai Uhuru eneo la Afrika ya Mashariki na Kati (Pafmeca) alitumwa Zanzibar kujaribu kuvusuluhisha vyama vya ZNP na ASP vilivyokuwa katika mgogoro.
Sura ya mgogoro huo wa vyama viwili vya siasa vya Zanzibar ambavyo Chiume alitumwa kuja kuusuluhisha mwaka 1958, una sura inayofanana na ile ambayo leo hii inawaweka katika meza moja viongozi wa vyama vikuu viwili vya siasa CCM na CUF kwa tatizo la Zanzibar.
Mwanademokrasia wa Kweli
Wakati vuguvugu la kudai mfumo wa vyama vingi lilipopamba moto nchini mwake, akifanya kazi kutoka hapa nchini, Chiume hakulala hadi alipounda chama chake na hatimaye kurejea nchini.
Aliporejea nchini mwake kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1994, vyombo vya habari vya huko vilikuwa vikimtaja kuwa Mmalawi maarufu kuliko wengine wote waliopata kuishi uhamishoni na mpinzani mkubwa kabisa wa Rais wa wakati huo wa Banda.
Chama chake cha upinzani alichokianzisha cha Congress for Second Republic na jitihada zake za kuviunganisha vyama kadhaa vidogo nchini huko mwaka 1996 ili kukabiliana na utawala wa aliyekuwa Rais wa Pili wa Malawi, Bakili Muluzi ni sehemu ya mambo yanayoonyesha namna alivyoheshimu misingi ya kidemokrasia.
Watanzania tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwa mzee wetu huyu ambaye kuondoka kwake kwa hakika kunaendelea kuwamaliza waasisi wa ukombozi wa mataifa yetu.
Leo hii serikali ya Rais Mbingu wa Mutharika wa Malawi inapokubali kumpa heshima zote za kitaifa Chiume katika mazishi yake, angalau pazia linaonekana kuanza kufunguka.
Hali ya matumaini inarejea na kwa kweli tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwa viongozi wa aina ya Chiume ambao hawakupata kulewa madaraka, ambao kwao Afrika ni taifa moja na ambao kwao uzalendo maana yake moja, kuwapigania, kuwatetea na kuwalinda watu wako.
Watanzania wanaoishi leo hii ni mashahidi wa namna viongozi wetu wengi wanavyofikiria zaidi matumbo yao na yale ya familia zao kuliko watu wanaowaongoza.
Kwa hakika tunapoyaangalia maisha binafsi na ya kisiasa ya wanasiasa wa kariba ya Chiume, tunapaswa kuyafanya kuwa masomo bora ya namna viongozi wetu wanavyopaswa kuishi leo na kesho ili huko tuendako waweke alama za uongozi uliotukuka na wa kuigwa.
Ingawa Chiume amefariki dunia, tunaamini kilio anacholiliwa, na Watanzania, Wamalawi, Waafrika wazalendo na ulimwengu mzima wa wapigania haki ni ushahidi kuwa mema aliyoyatenda yameacha alama ya aina yake.
Kwa hakika kifo chake kimethibitisha Chiume hapaswi kuliliwa kwa kusononeka na kwa kwikwi tu, bali tuna wajibu wa kulia kilio cha kumpoteza shujaa, mwana adhimu wa Afrika, mtetezi wa wanyonge, mpenda haki na shahidi wa mapambano yetu.
Tujifunze kutoka kwa Kanyama Chiume
NI wiki moja kamili sasa tangu Afrika impoteze mmoja wa majemedari wake wa mwisho na mwasisi wa mapambano ya uhuru na umoja wa kweli wa Afrika, Mzee Kanyama Chiume akijulikana kabla ya hapo kama, Murray William Kanyama Chiume (78).
Mzee Chiume alifariki dunia Jumatano iliyopita akiwa New York Marekani, ambako alikuwa akiishi kwa miaka kadhaa na baadhi ya watoto wake walio huko kikazi.
Kwa hakika kifo cha shujaa huyu wa Malawi, Tanzania na Afrika nzima kinalifanya bara hili kuendelea kupoteza baba mmoja baada ya mwingine wa vita vya ukombozi na waasisi wa mapambano ya umoja wa Afrika.
Kabla ya kifo chake cha wiki iliyopita, Afrika ilikuwa imebakiwa na yeye na Rais wa zamani wa Zambia, Kenneth Kaunda.
Bila ya kutafuna maneno, viatu vya Chiume vilikuwa vikiwatosha wanasiasa wa kariba yake; akina Kwame Nkrumah, Julius Nyerere, Jomo Kenyatta, Sekou Toure na wachache wengine ambao idadi yao haizidi wanafunzi 12 wa Yesu Kristo.
Wakati Baba wa Taifa alipokuwa ndiye kiongozi wa harakati za mapambano ya uhuru wa Tanganyika miaka ya mwanzoni mwa 1950, Chiume ndiye aliyekuwa kinara nchini Malawi, akiwa ndiye mwakilishi wa chama cha Nyasaland Congress Party kilichokuja kujulikana baadaye kama Malawi Congress Party.
Kupitia katika chama chake hiki, yeye ndiye aliyekiwakilisha katika mikutano ya kimataifa kule London, Accra Ghana na Tanzania.
Alishiriki kikamilifu katika uanzishwaji wa vuguvugu la kudai uhuru kwa pamoja kwa mataifa ya Kiafrika akiwa mjumbe wa Malawi katika mkutano uliozaa lile la nchi zilizo Afrika ya Mashariki na Kati (Pafmeca) kule Mwanza na baadaye Pafmecsa ukijumuisha na nchi za kusini.
Alikuwa miongoni mwa viongozi wa Kiafrika waliokutana mara kadhaa kwa ajili ya kuanzisha uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU) na mwaka 1964 katika mkutano uliofanyika Cairo Misri, hotuba kali ya kimapinduzi ndiyo iliyomkera rais wake Kamuzu Banda na kumjenga uhasama.
Nilipokutana naye kwa mara ya kwanza, Mzee Chiume alipata kunisimulia kuhusu mzozo mkali wa maneno uliozuka kati ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Rais wa Kwanza wa Ghana, Kwame Nkrumah ambao ulitishia uhai wa OAU.
Leo hii miaka takriban 10 tangu anieleze kuhusu tukio hilo alilolielezea kuwa ni baya kuliko yote katika uhai wa OAU, bado naweza nikakumbuka kwa ufasaha maneno aliyonieleza.
“Bado naikumbuka siku hiyo vyema kabisa. Ilikuwa ni siku ngumu kwetu. Viongozi wetu wawili, tuliokuwa tukiwaheshimu na kuwasikiliza, walizozana kweli kweli. Mwalimu alikuwa akipinga mtazamo. Sijapata kumuona Mwalimu akiwa amekasirika kama siku hiyo. Ugomvi ule ungeweza kuimega OAU,” alinieleza Chiume aliyekuwa akizungumza Kiswahili kwa ufasaha kabisa huku akivuta tukio moja baada ya jingine.
Katika mazungumzo yake siku zote, Chiume alikuwa akiiona Afrika kuwa moja na mipaka ya kikoloni haikuwa kikwazo cha kuwafanya Waafrika kupigana.
Ninapokumbuka maneno mengi mazito niliyoyasikia kutoka kwa Chiume miaka 1o iliyopita na kupekua pekuwa makabrasha ya historia ya bara hili, kwa mfano wa maneno ya Yohana Mbatizaji, napata shida kuwafunga kidamu za mzee huyo viongozi wa zama hizi wa Bara la Afrika.
Watoto wadogo na Watanzania wasioijua vyema historia ya mapambano ya uhuru wa Malawi na ile ya Afrika ya kati ya miaka ya 1950 hadi 1960 wanaweza wakashangaa, jina la mwanasiasa huyu likitajwa na kuwekwa katika mizania ya wanasiasa wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere.
Chiume na wenzake wengine kadhaa akiwamo rafiki yake mkubwa Henry Chipembere na Orton Chirwa wanaweza wakatajwa kuwa ndiyo viongozi waasisi wa mapambano ya uhuru wa Malawi.
Chiume ambaye miaka ya mwanzoni mwa 1950 alikuwa na umri usiodizi miaka 25 na wenzake zama hizo wakijulikana kwa jina kwa jina la Kiingereza ‘The Young Turks’ (Vijana wasiodhibitika).
Nilipokutana naye katika kipindi cha kati ya mwaka 1996 wakati huo akija hapa nchini mara kadhaa baada ya kurejea Malawi miaka miwili iliyotangulia, nilipata fursa ya kujifunza mambo mengi kuhusu maisha ya mwanasiasa huyu na namna alivyoshirikiana na wenzake wengine katika vita ya mapambano ya ukombozi wa Afrika.
Mzee Chiume alinipa fursa ya kuijua historia ya Malawi, Tanzania na Afrika, nje ya ile tunayosoma katika vitabu na maandiko mabalimbali ya kihistoria.
Ndani ya akili yake, mzee huyo ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 66, alikuwa na kumbukumbu sahihi ya matukio mbalimbali yaliyokuwa yakitokea zama za harakati za kudai uhuru wa nchi yake na ule wa Afrika.
Kwa hakika nikiwa mwanafunzi wa historia zama hizo, mzee huyu aliongeza ufahamu wangu kuhusu historia iliyopotoshwa ya harakati za ukombozi wa bara la Afrika.
Kupitia kwake nilimfahamu Kamuzu Banda, Rais wa kwanza wa Malawi ambaye miaka 30 ya utawala wake wa kiimla, aliiondoa nchi yake kuwa miongoni mwa mataifa ya mwanzo kabisa kudai na kupigania uhuru si wa taifa moja moja la Afrika bali la Afrika.
Kwa maneno yake mwenyewe Mzee Chiume aliniambia kuwa alikuwa akijutia uamuzi wake yeye na mwenzake Chipembere wa kusikia ushauri wa aliyekuwa Rais wa Kwanza wa Ghana, Kwame Nkrumah wa kuwataka wao wamkubali Banda kuwa kiongozi wa harakati zao za ukombozi wa Malawi.
Wakiwa wadogo kiumri, Chiume na Chipembere waliheshimu maoni hayo ya Nkrumah wakihadaika na ushiriki wa Banda katika harakati za mwanzoni kabisa za mshikamano wa Waafrika (Pan African Movement).
Kama ilivyokuwa kwa Nkrumah na kwa vijana hao ambao walikuwa wameshaasisi mapambano ya uhuru wa nchi yao, Banda wa zama hizo, miaka ya 1940 na 1950 alibeba taswira ya kweli ya mwana wa Afrika, mpigania uhuru mwenye uchungu na nchi yake na bara lake.
Ni jambo la bahati mbaya kwamba, uamuzi wa Banda kuhudhuria mkutano wa kwanza wa Mwamko wa Afrika (PanAfrican Congress) mwaka 1945 kule Manchester, Uingereza akiwa na Kenyatta na Nkrumah ulimfanya aonekane kuwa mmoja wa wanamapinduzi hodari na wa kuaminika wa Kiafrika. Ukweli haukuwa huo.
Mzee Chiume alinieleza namna Banda alivyoweza kutoka ndani ya gamba alilojificha kwa zaidi ya miaka 10, kwnai miezi isiyozidi mitatu tangu Malawi ipate uhuru wake mwaka 1964, ghafla alibadilika na akawa mpinzani mkubwa wa misingi ya ukombozi wa taifa lake na ule wa bara lake.
Akina Chiume walipigwa na butwaa kumuona Banda akitangaza kuutambua utawala wa kibaguzi wa makaburu wa Afrika Kusini ambao ulikuwa umetengwa na jumuiya ya kimataifa na miaka michache baadaye akaingia katika mzozo na Tanzania akigombea sehemu ya ardhi yetu.
Chiume, wakati huo akiwa Waziri wa Mambo ya Nje akiungwa mkono na mawaziri wenzake wengine watano, walikataa kumtii Banda, na matokeo yake wakafukuzwa kutoka serikalini.
Hali hii haikuishia hapo, Banda ambaye alishawatangaza kuwa ni wasaliti, akafanya jaribio la kuwakamata na kuwaua, tukio ambalo liliwanasa watu kadhaa na kumkosa Chiume ambaye kwa msaada wa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere alifanikiwa kutorokea Tanzania.
Kama ilivyokuwa kwa wana mapinduzi wengine kadhaa wa Kiafrika Chiume akarejea Tanzania ambako alisomea na kukulia na akaishi katika kipindi chake chote cha miaka 30 akiwa mkimbizi.
Nilipozungumza naye kuhusu matukio hayo, Chiume alikiri kufanya kosa kubwa la kumruhusu Banda kuziteka nyara harakati zao za mapambano ya uhuru wa Malawi nay ale ya Afrika.
Kwa hakika, kama si hulka yake ya kutopenda madaraka na kuwa tayari kusikiliza ushauri wa wanamapinduzi wenzake, Chiume alikuwa na nafasi kubwa ya kuwa Rais wa kwanza wa Malawi huru na mmoja wa viongozi ambao kifo chake kingewekwa katika daraja moja na akina Nyerere na Nkrumah hata na wale ambao hawakupata kumfahamu.
Wakati nikizungumza naye miaka 10 iliyopita, kulikuwa na maneno ya chinichini yalikuwa yakidai kuwa, Banda halisi aliyechukuliwa na Waingereza na kupelekwa Afrika Kusini na baadaye Uingereza hakuwa yule yule aliyerudi Malawi na kuwa Rais wa Kwanza wa Taifa hilo dogo lililo Kusini Mashariki mwa Afrika.
Nilipozungumza naye kuhusu tetesi hizo, Mzee Chiume alinihakikishia kuwa alikuwa ameshaanza kulifanyia uchunguzi suala hilo na kimsingi alitaka kuandika kitabu juu ya kile kilichotokea Malawi na hadaa ya Banda iliyomwezesha kuupata urais wa Malawi. Sikupata kujua iwapo alitimiza lengo lake hilo.
Amefariki akiwa na mapenzi makubwa kwa taifa lake na kwa Bara lake na ndiyo maana aliporejea nchini mwaka 1994, alianzisha chama cha upinzani akikiita Congress for Second Republic (CSR), akiamini kuwa taifa hili lilikuwa likihitaji uhuru wa kweli.
Tangu wakati huo akawa mstari wa mbele kupigania uimara ya mfumo wa vyama vingi na akatumia muda wake mwingi kuwaasa Wamalawi wenzake kutokubali tena kuirejesha nchi yake katika udikteta wa chama kimoja. Utawala wa mkono wa chumba wa Banda ukampa fundisho kubwa.
Tanzania
Chiume hawezi kutenganishwa na Tanzania. Historia yake ya maisha yake binafsi, kifamilia na kisiasa yanaungana moja kwa moja na taifa hili.
Mwandishi mwenzangu Maggid Mjengwa katika blogu yake ameonyesha kwa ufasaha namna Mzee huyu alivyo na uhusiano na taifa hili. Maggid anaanza kwa kusema;
Huyu mzee alisoma katika shule mbalimbali hapa nchini kuanzia elimu yake ya msingi hadi ile ya Sekondari kabla ya kwenda Chuo Kikuu cha Makerere alikosomea ualimu.
Aidha hata alipokuja kuishi ukimbizini, alioa mke wa Kitanzania akazaa watoto wake akina Nathan na ndugu zake wengine Tanzania. Wamesoma Tanzania na kimsingi wana Utanzania.
Akiwa ukimbizi hapa nchini, Chiume alikuwa akifanya kazi ya uandishia na makala zake za kimapinduzi zilikuwa zikichapwa katika magazeti mbalimbali kuanzia The Nationalist (baadaye Uhuru na Mzalendo) na katika gazeti la serikali la Daily News.
Si hayo tu, hata kabla ya uhuru wa Malawi, Chiume akiwa mjumbe wa Vuguvugu la Kudai Uhuru eneo la Afrika ya Mashariki na Kati (Pafmeca) alitumwa Zanzibar kujaribu kuvusuluhisha vyama vya ZNP na ASP vilivyokuwa katika mgogoro.
Sura ya mgogoro huo wa vyama viwili vya siasa vya Zanzibar ambavyo Chiume alitumwa kuja kuusuluhisha mwaka 1958, una sura inayofanana na ile ambayo leo hii inawaweka katika meza moja viongozi wa vyama vikuu viwili vya siasa CCM na CUF kwa tatizo la Zanzibar.
Mwanademokrasia wa Kweli
Wakati vuguvugu la kudai mfumo wa vyama vingi lilipopamba moto nchini mwake, akifanya kazi kutoka hapa nchini, Chiume hakulala hadi alipounda chama chake na hatimaye kurejea nchini.
Aliporejea nchini mwake kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 1994, vyombo vya habari vya huko vilikuwa vikimtaja kuwa Mmalawi maarufu kuliko wengine wote waliopata kuishi uhamishoni na mpinzani mkubwa kabisa wa Rais wa wakati huo wa Banda.
Chama chake cha upinzani alichokianzisha cha Congress for Second Republic na jitihada zake za kuviunganisha vyama kadhaa vidogo nchini huko mwaka 1996 ili kukabiliana na utawala wa aliyekuwa Rais wa Pili wa Malawi, Bakili Muluzi ni sehemu ya mambo yanayoonyesha namna alivyoheshimu misingi ya kidemokrasia.
Watanzania tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwa mzee wetu huyu ambaye kuondoka kwake kwa hakika kunaendelea kuwamaliza waasisi wa ukombozi wa mataifa yetu.
Leo hii serikali ya Rais Mbingu wa Mutharika wa Malawi inapokubali kumpa heshima zote za kitaifa Chiume katika mazishi yake, angalau pazia linaonekana kuanza kufunguka.
Hali ya matumaini inarejea na kwa kweli tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwa viongozi wa aina ya Chiume ambao hawakupata kulewa madaraka, ambao kwao Afrika ni taifa moja na ambao kwao uzalendo maana yake moja, kuwapigania, kuwatetea na kuwalinda watu wako.
Watanzania wanaoishi leo hii ni mashahidi wa namna viongozi wetu wengi wanavyofikiria zaidi matumbo yao na yale ya familia zao kuliko watu wanaowaongoza.
Kwa hakika tunapoyaangalia maisha binafsi na ya kisiasa ya wanasiasa wa kariba ya Chiume, tunapaswa kuyafanya kuwa masomo bora ya namna viongozi wetu wanavyopaswa kuishi leo na kesho ili huko tuendako waweke alama za uongozi uliotukuka na wa kuigwa.
Ingawa Chiume amefariki dunia, tunaamini kilio anacholiliwa, na Watanzania, Wamalawi, Waafrika wazalendo na ulimwengu mzima wa wapigania haki ni ushahidi kuwa mema aliyoyatenda yameacha alama ya aina yake.
Kwa hakika kifo chake kimethibitisha Chiume hapaswi kuliliwa kwa kusononeka na kwa kwikwi tu, bali tuna wajibu wa kulia kilio cha kumpoteza shujaa, mwana adhimu wa Afrika, mtetezi wa wanyonge, mpenda haki na shahidi wa mapambano yetu.
