Na Absalom Kibanda
NCHI hii haiishi vituko. Kila siku inayokwenda kuna jambo jipya linaloibuka katika nchi hii na kufunika lile lililotangulia au lililotokea siku, wiki, miezi au miaka kadhaa iliyopita.
Katika siku za hivi karibuni, Watanzania tumeshuhudia kuibuka kwa mambo kadha wa kadha mazito yanayogusa mwenendo wa mambo kitaifa na pengine kuathiri kwa namna njema au mbaya mustakabali wetu kama nchi leo hii na katika siku zijazo.
Jambo la kwanza ambalo nimekuwa nikilitazamia katika hayo yote ninayofikiria ni lile linalogusa kesi zinazowakabili baadhi ya watuhumiwa wa wizi wa mabilioni ya fedha kutoka katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA) iliyokuwa ndani ya Benki Kuu ya Tanzania katika kipindi cha mwaka 2005.
Kufikishwa mahakamani kwa watuhumiwa 20, wote wakijimuishwa katika tuhuma mbalimbali ndani ya mtungi mmoja huo huo wa EPA wakiwamo wafanyabiashara wenye majina makubwa wa kiwango wa ‘Jeetu Patel’ kulifungua ukurasa mpya katika mapambano dhidi ya ufisadi, tatizo ambalo hakuna shaka limekuwa kitovu cha ulaji usiostahili kwa miaka mingi sasa.
Matukio ya kufikishwa mahakamani kwa watuhumiwa hawa yaliyozingira hisia na mwenendo wa mambo nchini kwa takriban wiki mbili, kulianza kuonekana kuwa ni mwanzo wa kikweli kweli wa mafanikio ya vita dhidi ya ufisadi iliyoanzishwa katika kipindi cha karibu mwaka mmoja na ushee uliopita.
Hata hivyo kama ilivyo ada, tukio hili la kufikishwa mahakamani kwa watuhumiwa hao, lilionekana kuligawa taifa katika makundi mengi kwa kiwango cha kusababisha kila kundi kuibua hoja zinazokinzana.
Kundi moja la wanaharakati wenye msimamo mkali kuhusu ufisadi, lilikataa na kimsingi limeendelea kukataa kukiona kitendo cha kufikishwa mahakamani kwa watuhumiwa hao 20 wa EPA kuwa hatua ya kwanza ya mafanikio ya serikali, Rais Jakaya Kikwete, wao wenyewe na vyombo vya habari ambavyo kwa pamoja vimekuwa vikipambana na vitendo vya ufisadi.
Kwa waumini wa kundi hili, mafanikio ya kweli kweli katika sakata hili la EPA yangeonekana iwapo tu, serikali na hususan Rais Jakaya Kikwete wangefumba macho na kuyafikisha mahakamani makampuni yote ambayo kwa namna mmoja au nyingine yalishiriki katika uchotaji wa shilingi bilioni 90 na ushee kati ya zile bilioni 133 zilizoibwa kutoka akaunti nzima ya EPA.
Kwa sababu hiyo basi, wanaharakati wa kundi hili walikuwa wakiamini kwamba, Rais Kikwete na serikali yake walikuwa hawana sababu hata moja ya kuwatenga wezi wa EPA katika makundi mawili ya wale waliorudisha fedha na wale ambao hawakurudisha na badala yake wote walikuwa wakipaswa kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria na kuiacha korti iamue hatima yao.
Kwa watu wa kundi hili, hatua ya serikali kutangaza msimamo wa kuwasamehe wale wote waliorejesha fedha, ilikuwa ina maana moja tu kwao; ‘usaliti katika mapambano dhidi ya ufisadi.’
Wafuatiliaji wasiopendelea upande wowote katika mapambano haya ya ufisadi ni mashahidi wazuri kwamba, uamuzi huu wa serikali kuwasamehe wale wote waliolipa fedha hizo ulizidi kuonekana usiofaa hasa baada ya taarifa kuanza kuvuja kwamba kampuni ya Kagoda Agriculture Ltd ilikuwa miongoni mwa makampuni yaliyokuwa yamefanikiwa kurejesha fedha zote kiasi cha shilingi bilioni 40 ilichochota EPA.
Taarifa kwamba Kagoda ilikuwa imefanikiwa kukwepa kitanzi na hatari ya kufikishwa kortini, ilikuwa ni habari mbaya kwa wanaharakati ambao kwao, kampuni hiyo ndiyo iliyokuwa ikistahili kubebeshwa mzigo takriban wote wa EPA pengine kabla ya mtuhumiwa mwingine wowote.
Joto la mtazamo wa wanahaerakati hao na mashabiki zao ndiyo ambayo imesababisha baadhi yao hadi leo hii kuendelea kuziona kesi zilizofunguliwa dhidi ya watuhumiwa wa EPA kuwa ni kiini macho na mchezo wa kuigizwa usio na lengo la kuikomboa nchi hii katika tatizo sugu la ufisadi.
Ni jambo la bahati mbaya sana kwamba, wanaharakati wa kundi hili wanaitaka serikali, Rais Kikwete na Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) kuchukua hatua za kuifikisha Kagoda mahakamani huku wakisahau ukweli wa wazi kabisa kwamba, kampuni hiyo ambayo usajili, mahali ilipo, wamiliki wake na namna ilivyochota fedha ni mambo yenye utata mkubwa inaonekana kuwa na uhusiano wa moja kwa moja wa siri na wa wazi na watu wenye mamlaka au waliopata kushika madaraka makubwa kabisa kidola.
Ni jambo la bahati mbaya sana kwamba, wanaharakati hawa wa ufisadi ambao kimsingi nayaunga mkono mapambano waliyoyaanzisha, wanasahau kabisa kile ambacho mwanazuoni wa siku nyingi na mwanasheria aliyebobea, Profesa Issa Shivji alipata kukisema kuhusu uhalali wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuendelea kuongoza nchi kikiwa katika taswira yake ya sasa ya chama dola.
Nasema hivi kwa sababu utafiti wangu binafsi kama mwanahabari na mtu ambaye katika kipindi cha miaka takriban 10 ya kazi yangu hii nimepata kukutana na kuzungumza na watu kadha wa kadha wakiwamo wale wanaohusishwa na Kagoda umenithibitishia pasipo shaka kwamba kampuni hii inayotajwa, ilianzishwa kwa utaratibu haramu ulioratibiwa na dola na kusimamiwa na baadhi ya viongozi wa juu serikalini na makada wenye nguvu ndani ya CCM.
Ni kwa sababu hiyo basi, ushahidi wa mazingira unaonyesha pasipo shaka kwamba, Kagoda ni jinamizi ambalo mizizi yake ilijengwa na uharamu uliokipa chama tawala uhalali wa kuendelea kuongoza nchi hii, kikiwa na sura yake ile ile ya CCM iliyostawi katika mizingira ya kidikteta yaliyorithiwa na vyama vya kisoshalisti na kikomunisti duniani zama za vita baridi.
Hakuna shaka kwamba, Kagoda katika maelezo ya kisomi, ni mfano wa taasisi za kifisadi, iliyojengwa ikihusisha dola na chama tawala ambavyo uhalali wa ubia wao uliwashirikisha wafanyabiashara marafiki na makada wakubwa wa CCM.
Mahusiano haya ndiyo ambayo kwa kiwango kikubwa yalisababisha serikali kushikwa na kigugumizi mapema kabisa sakata hili la EPA lilipoanza hata kufanya jitihada za kununua muda kwa kuhalalisha makampuni makubwa mawili ya kimataifa ya ukaguzi wa mahesabu, kwanza Delloite & Touche na kisha Ernst & Young kuyapitia mahesabu ya BoT na EPA na kisha kuwasilisha taarifa zake serikalini.
Ni jambo la ajabu kwamba, hata baada ya Delloite & Touche kupitia mahesabu na kubaini wizi uliofanywa na Kagoda na makampuni mengine na serikali kuamua kuipa kampuni nyingine kazi ile ile, wanaharakati hawa wenye msimamo mkali walihadaika na kuipa dola nafasi nyingine ya kujipanga na kutafuta majibu ya namna ya kujinusuru.
Ni jambo la ajabu kwamba, wanaharakati hawa hawa, walikaa kimya na wakashindwa kutambua nini maana ya yote hayo ilhhali katika kumbukumbu zao wakiwa na barua mbili zenye kupingana zilizoandikwa katika kipindi kisichozidi wiki moja na aliyekuwa Waziri wa Fedha na Uchumi, Zakia Meghji kuhusu sakata hilo hilo la EPA.
Ni ukweli rahisi kabisa kwamba, iwapo wanaharakati wangekuwa wakiunganishwa na chombo chenye sauti moja kuhusu jambo hili, wangebaini mapema kabisa kwamba, Meghji aliingizwa katika mtego wa barua mbili zinazokinzana si kwa sababu ya udhaifu wake, bali kutokana na shinikizo la kidola ambalo lilikuwa likimtaka yeye kama Waziri wa Fedha kufanya lolote lililokuwa likiwezekana kuinusuru serikali, chama chake na baadhi ya watu wenye mamlaka ambao kwa namna moja au nyingine walitumia madaraka yao vibaya kuihalalishia CCM ushindi mwaka 2005.
Leo hii wanapoibuka kwa ujasiri mkubwa, akina Reginald Mengi, Dk. Willibrod Slaa, Zitto Kabwe, M.M Mwanakijiji, Mpayukaji, wanaharakati na wanasiasa wengine wengi makini wakitaka siri ya Kagoda ifichuke, kwa hakika hoja zao zinazidi kuongeza mtihani kwa serikali ambayo imenunua muda mwingi na kutumia kila aina ya mbinu kuinusuru kampuni hii.
Unapoziangalia juhudi zote hizi za serikali za kuinusuru Kagoda, kwani wakifanya siri taarifa zote za ukaguzi wa mahesabu ya BoT, hata baada ya nyingine kuonekana zimevuja, pili wakitumia kamati ya Mwanyika ambayo hadi leo hii matokeo yake ni kitendawili na tatu wakijaribu kujificha nyuma ya madaraka makubwa ya kisheria ya DPP, ndipo siri na nini hasa kinachofichwa kinapojulikana.
Kwa hakika leo hii angetokea Mengi, Slaa, Mwanakijiji na Mpayukaji wakaniuliza ni jambo gani bora unalodhani linatupasa Watanzania tulifanye ili kujua kwa uhakika siri iliyojificha ndani ya Kagoda, sintapita na kuanza kutaja orodha ya wamiliki wa kampuni hiyo tata bali jicho langu na akili yangu nitaielekeza CCM moja kwa moja.
Nasema hivi kwa sababu naamini tena kwa dhati kabisa kwamba, Kagoda ni mchezo mchafu wa CCM ambao ulitumika kukirejesha madarakani isivyo halali chama hicho tawala mwaka 2005 kikinunua mioyo ya watu kwa fedha haramu hata kuwapa udiwani, ubunge na urais.
Kwa sababu hiyo basi, kwangu mimi Kagoda si mtu mmoja, wawili watatu au wanne, bali ni mkakati wa miaka mingi, wa CCM na serikali yake wa kufuja matrilioni ya fedha ambazo malengo yake ya msingi ni kuwahudumia wananchi wanaoishi maisha yaliyozongwa na tabu ambazo kimsingi hawastahili.
Kwa sababu hiyo basi, jibu langu kwa Mengi lingekuwa mdudu Kagoda anayetafuta jibu lake ni tunda la uasi lililostawishwa kikatiba na kuipa CCM mamlaka ya dola ambayo yamkini mafisadi wachache wanaopewa baraka na dola wamekuwa wakiyatumia kufuja na kuimaliza nchi hii.
Kwa hakika staili iliyotumiwa na CCM na serikali yake kuhalalisha wizi BoT mwaka 2005 ndiyo ambayo ilitumika wakati serikali ilipoliingiza taifa katika mradi tata wa Richmond ambao uligharimu madaraka ya watu wachache sana serikalini ambao mpaka kesho naendelea kuamini walitolewa kafara ili kukinusuru chama hicho na fedhaha ya kuanguka kizima kizima.
Watanzania tunapaswa kutambua kwamba, staili hii ya CCM ya kujivua gamba nusunusu na kuwatoa kafara wachache miongoni mwa mafisadi wengi walio ndani ya chama na serikali yake, ndiyo ambayo imekuwa ikikijengea uhalali wa kuendelea kuwahadaa wananchi wenye mapenzi ya kweli na taifa lao.
Ni kwa sababu ya kuifahamu CCM kwa jicho hilo ndiyo maana hadi leo hii nimekuwa ni mtu wa mwisho kushangilia kuanza kusikilizwa kwa kesi za EPA, kufikishwa mahakamani kwa Basil Mramba na Daniel Yona mahakamani na kabla ya hapo kulazimishwa kujiuzulu kwa Edward Lowassa, Nazir Karamagi, Andrew Chenge na.
Kwangu mimi mafanikio ya kweli ya vita dhidi ya ufisadi yataanza wakati Watanzania watakaposimama na kuacha kushangilia siasa za msimu na kuzika madhambi za wana CCM kulana wenyewe kwa wenyewe (Political Cannibalism) ama kwa kulazimishana kujiuzulu, kusutana, kunyosheana vidole, kutishana na kuburuzana mahakamani ilhali chama kinachotoa baraka za wizi huo kuendelea kikiendelea kubakia madarakani kikiwa na sura za watu wale wale wanaohamishana kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Huko ndiko tunakopaswa kwenda.

